Home » » UMMY ‘AKOMALIA’ DAWA VITUO AFYA

UMMY ‘AKOMALIA’ DAWA VITUO AFYA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



WAZIRI wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, amewataka waganga wakuu wa wilaya nchi nzima kuhakikisha vituo vya afya kunakuwa na dawa za kutosha.
Miongoni mwa dawa hizo ni ya kuongeza damu kwa wajawazito iitwayo Foriki Asidi na dawa ya usingizi na kuonya kuwa kiongozi wa kituo cha afya ataadhibiwa kujiuzulu kama kituo kitabainika kutokuwa na dawa hizo.

Alitoa agizo hilo jana wakati akikabidhi gari la kubeba wagonjwa lenye thamani ya Sh. milioni 200 kwa Kituo cha Afya cha Pongwe pamoja na magodoro 25, mashuka 25 na vitanda 25 kwa lengo la kurahisisha huduma kwa wagonjwa.
“Haiwezekani serikali inatenga mabilioni ya fedha katika vituo vya afya halafu unakuta wagonjwa hususan wajawazito na watoto

wanapoteza maisha kwa sababu kukosekana kwa dawa, hivyo mganga mkuu atakayekutwa hana dawa hizo muhimu anapaswa kujiuzulu mara moja,” alisisitiza.


“Sitavumilia kuona hali hiyo kamwa, lazima waganga wakuu wajiuzulu endapo watashindwa kusimamia fedha za serikali kununua dawa za kutosha na kuzisambaza katika vituo vya afya ili kuwaondolea usumbufu wananchi na kupunguza vifo vitokanavyo na upungufu wa dawa na vifaa tiba kwa wajawazito,” aliongeza.

Ummy aliwaelekeza kwa wakuu wa wilaya na wakurugenzi wa halmashauri nchini kuhakikisha katika vituo vya afya kunakuwa na dawa za kutosha kwani serikali imewekeza fedha nyingi ili kuhakikisha wananchi wanakuwa na afya bora.

“Ndugu zangu afya ni mtaji, lazima serikali tuwekeza katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora ili kunusuru vifo visivyo vya lazima,” alisema Ummy.  

Aliwaeleza wananchi wa Pongwe kuwa atahakikisha anatokomeza vifo vya wajawazito na watoto alipoapishwa na Rais John Magufuli, hivyo atahakikisha anasimamia suala hilo kikamilifu na mtumishi atakayebainika kudhoofisha jitihada za maendeleo katika upatikanaji wa dawa, atamchukulia hatua kali ikiwamo kumfukuza kazi na kumfutia usajili wa kibali cha kupata kazi mahali pengine.

Alisema serikali ya awamu ya tano ilipoingia madarakani ilikuta bajeti ya fedha za mahitaji ya dawa kila mkoa ilikuwa Sh. bilioni 1.1, lakini mwaka wa pili alipandisha na kuweka bajeti ya Sh. bilioni 3 na mwaka uliofuata amepandisha bajeti hiyo hadi Sh. bilioni 4.3 ambayo ilipitishwa mwaka huu wa fedha.

Alisema fedha hizo zimepatikana kutokana na juhudi ya kuwabana wapigadili na kununua dawa moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji.
 
Diwani wa kata ya Pongwe, Mubaraka Sadi, alimshukuru Waziri Ummy kwa kuwapatia msaada wa gari pamoja na vifaa mbalimbali kwa kuwa kinamama wamekuwa wakipoteza maisha wakiwa njiani kufuata huduma za afya kutokana na ukosefu wa gari la kubeba wagonjwa kuwapeleka Hospitali ya Rufani ya Bombo.

Chanzo Nipashe

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa