Home » » `Maji Marefu` akitahadharisha CCM

`Maji Marefu` akitahadharisha CCM

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mbunge wa Korogwe Vijijini (CCM),Stephen Ngonyani.
 
Mbunge wa Korogwe Vijijini (CCM),  Stephen Ngonyani,  ametahadharisha kuwa tamaa ya  fedha na madaraka ndivyo visu viwili vitakavyoichinja  CCM  kwani  viongozi waliotoa  fedha  kununua  madaraka  hawajali matatizo ya  wananchi wenye maisha duni.
Kiongozi huyo Stephen  Ngonyani, mbunge wa Korogwe Vijijini alisema kutokana na kutojali shida za wananchi wengi maskini baadhi ya Watanzania wamejenga chuki baina ya masikini wa kipato  na wale wenye nacho.

Ngonyani maarufu kama Profesa Maji Marefu alisema  wanachama hao wachumia tumbo watakiathiri chama kwa kuwa wamewaacha walalahoi wakiteketea  kwa magonjwa  na  umasikini, huku wao wakiponda raha kwa kula kodi za wavuja jasho.

Mbunge huyo alisema hayo wakati akiwahutubia  wapigakura  wake katika  mikutano mbalimbali ya hadhara anayoifanya jimboni humo kuhamasisha  shughuli za maendeleo na kutatua kero za wananchi.

Alionya kuwa hali hiyo inawafanya wanachama wa chama hicho na wananchi wengine   kudhani kuwa mwenendo  wa  viongozi  hao kutowajali watu  ndiyo maelekezo ya chama  jambo alilolieleza kuwa linasababisha watu kuichukia  CCM na serikali yake.

“Tamaa ya fedha na uchu wa madaraka ni sumu kubwa ndani ya chama hiki, wenye fedha wameingia madarakani kwa ajili ya malengo yao,  mengi  mazuri yanayofanywa na serikali  hawataki  kuyazungumza ,  kazi yao ni majungu, fitina na uongo  na  wamewasahau   wananchi” alionya Ngonyani.

Aidha aliwataka wananchi kutochanganya  urafiki  ama itikadi katika masuala ya maendeleo  na kwamba CCM  siyo mbaya  lakini baadhi ya viongozi ndiyo  tatizo na chimbuko la watu wanaokichukia chama hicho  na kudiriki hata kukihama na kuhimiza  upendo, umoja na  mshikamano  ili kuondoa  dosari  zenye kukichafua  chama  hicho.

Mjumbe wa Halmashauri  ya CCM  Wilayani Korogwe, Shebila  Idd  alieleza kuwa  kiongozi  anayetosha  ni yule  mwenye kubaini  udhaifu  na utendaji  wa mwenye mamlaka  na kutafuta  ufumbuzi  na kwamba asiwe wa  kuzungumza upungufu  wa mtu huyo  kwenye  vijiwe ambavyo vina watu wa itikadi tofauti .

Idd  diwani  wa kata ya Kerenge na Mwenyekiti  wa Kamati  ya Huduma za Jamii  katika Halmashauri  ya Korogwe Vijijini, aliwataka viongozi  kuonyesha  njia  na kwamba Watanzania  watawapima  kutokana na  matendo yao.
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa