Home » » Kamati yavunja nyumba

Kamati yavunja nyumba

KAMATI inayosimamia migogoro ya ardhi na viwanja katika eneo la Kange Kasera jijini Tanga imevunja nyumba mbili zilizojengwa kinyume cha utaratibu na wavamizi waliovamia bila ya kufuata utaratibu.
Zoezi hilo ambalo limesimamiwa na Ofisa Tarafa ya Pongwe, Juma Msagati, umefanyika baada ya kamati hiyo kutoa taarifa ya kuvamiwa eneo la viwanja ambalo bado lina mgogoro na kuanza kujengwa isivyo halali.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya zoezi hilo, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Dickson Mhando, alisema kuwa wamefikia hatua hiyo baada ya wahusika kwenye viwanja vya wamiliki wengine pasipo kufuata taratibu.
“Eneo la Kange Kasera lipo kwenye mgogoro wa viwanja, lakini upo katika hatua za mwisho za kupata ufumbuzi sasa kuna watu wameanza kuvamia maeneo na kujenga bila kufuata taratibu wakati eneo bado lina mgogoro, hivyo tumeamua kuvunja,” alisema Mhando.
Alisema kuwa wameamua kuchukua hatua hiyo ili kama kuna wavamizi wengine wana nia kama hiyo waache hadi hapo utaratibu wa upimaji wa maeneo utakapokamilika.
Hata hivyo, Msagati alisema kuwa kabla ya wavamizi hao kuchukuliwa hatua za kubomolewa nyumba hizo, waliwataka wazivunje kwa hiari yao kabla ya hatua zaidi hazijachukuliwa.
“Nilitoa taarifa kwa njia ya barua kusitisha ujenzi wa nyumba zao kutokana na eneo wanalojenga kutokuwa mali yao, lakini walikataa kufanya hivyo ndiyo maana tupo hapa na kamati kuvunja nyumba hizo kutokana na kutoitikia wito,” alisema Msagati.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa