Home » » Halmashauri za mfano CHF kuzawadiwa

Halmashauri za mfano CHF kuzawadiwa



HALMASHAURI zitakazoandikisha kaya nyingi kuingia kwenye Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) zitazawadiwa kitaifa kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) imefahamika.
Ahadi hiyo ilitolewa juzi na mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa NHIF, Dk. Raphael Chegeni, wakati wa mkutano wa siku ya wadau mkoani Tanga ulioitishwa na mfuko huo katika utaratibu wake wa kukutana na wadau ngazi ya mkoa.
Dk. Chegeni alisema tayari menejimenti ya mfuko imeagizwa kuharakisha mapendekezo hayo ili yawasilishwe kwenye bodi kwa uamuzi.
Kwa mujibu wa mjumbe huyo, hatua hiyo itakaporidhiwa itachochea matokeo makubwa kufikia lengo la afya bora kwa wote na kuleta hamasa mpya katika utekelezaji wa huduma za CHF ngazi ya halmashauri.
Aidha, aliutaka uongozi wa NHIF kushirikisha wadau katika hatua muhimu za matayarisho ya tuzo hiyo ili kuleta mvuto na matokeo bora.
Dk. Chegeni alishauri kwamba jopo litakalotafuta washindi litokane na wadau wenyewe.
Akipongeza hatua hiyo, Maimuna Singano, ambaye ni mdau wa afya mkoani hapa alitaka wigo uongezwe kwa kuwa wapo watendaji wa kata na vijiji wanaofanya kazi ya kuhamasisha wananchi kuhusu CHF lakini juhudi zao hazijatambuliwa.
Naye Mkurugenzi wa tathmini ya uhai wa NHIF, Michael Mhando alizitaja halmashauri zinazofanya vizuri katika usimamizi wa huduma za CHF ni Iramba, Singida Vijijini, Meru, Rombo, Igunga na zote za Mkoa wa Tanga.
Mara ya mwisho NHIF kutoa tuzo ilikuwa mwaka 2012 ambapo baadhi ya halmashauri na mashujaa 50 wa mfuko huo wakiwemo waandishi wa habari walitunukiwa tuzo hizo na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, wakati mfuko huo ulipoadhimisha miaka 10 ya kuasisiwa kwake.

Chanzo;Tanzania daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa