Home » » Wafanyakazi Afritex wagoma

Wafanyakazi Afritex wagoma

WAFANYAKAZI zaidi ya 500 wa kiwanda cha nguo Afritex Limited, mkoani hapa, wamegoma kufanya kazi hadi mkuu wa idara kiwandani hapo atakapofukuzwa kazi.
Wakizungumza na Tanzania Daima jana, wafanyakazi hao walisema hawamtaki mkuu huyo wa idara, Uchit Jha, kwa madai amekuwa akiwanyanyasa kwa kuwatolea lugha chafu.
Mmoja wa wafanyakazi hao, Ferouz Hussein, alisema Jha amekuwa pia akiwakata mishahara bila sababu, hivyo kuwasababishia kutofanya kazi kwa uhuru na amani.
Naye Halima Juma alisema unyanyasaji unaofanywa na mkuu huyo wa idara umekuwa ukizidi kila kukicha, hivyo kumtaka meneja wa kiwanda hicho kumfukuza kazi.
Rajabu Mgaya alisema kuwa si kwamba wamegomea kazi bali wamegoma kufanya kazi na mkuu wa idara huyo ambaye aliwahi kufanya kazi kiwanda cha KTM Dar es Salaam na kufukuzwa kwa vitendo vyake vya unyanyasaji kwa wafanyakazi.
Meneja wa kiwanda hicho, Prakash Kunnur, alisema hajayapata malalamiko hayo na kwamba yakimfikia atayafanyia kazi ili kuondoa mgogoro uliopo.
“Kwa sasa siwezi kujua kama malalamiko hayo hayana ukweli au la kwa kuwa sijapokea malalamiko yoyote kutoka kwa wafanyakazi ila nitalifanyia kazi na mambo haya hayatajirudia tena,” alisema Kunnur.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa