Home » » Diwani atuhumiwa kuhujumu maji ya kijiji

Diwani atuhumiwa kuhujumu maji ya kijiji

WAKAZI wa Kata ya Mbuzee, wanamtuhumu Diwani wao, Rashid Shewedi (CCM), kuhujumu miundombinu ya maji na kujipatia kipato.
Wakizungumza na Tanzania Daima baadhi ya wanakijiji walisema wamekuwa wakikosa maji safi na salama huku maji hayo yakiwanufaisha watu wachache, akiwamo diwani huyo, anayeyatumia kwa kuyauza.
“Tanki ka maji la kijiji halina uwezo wa kugawa maji kwenye mikondo mingi, lakini diwani ameruhusu mikondo zaidi ya 70 ambayo maji yake yanakwenda huko kwa masilahi yake binafsi na sisi wananchi kukosa maji hayo na badala yake tunayafuata umbali mrefu,” alisema Ahmed Shemela.
Wanakijiji hao waliongeza kuwa licha ya kuyafuata umbali mrefu, maji hayo si salama.
“Maji tunayotumia ni ya Mto Soni, nayo si salama, vinyesi vya chooni vinaingia humo na tunatumia muda mwingi kuyafuata,” walisema.
Akizungumzia tuhuma hizo, diwani huyo alikiri kuwapo kwa tatizo la maji kwenye kata yake na kukana tuhuma zilizoelekezwa kwake.
Katika maelezo yake Shewedi alidai kuwa tatizo hilo ni kubwa na si kijiji kimoja, bali karibu vijiji vyote hivyo wapo mbioni kukarabati miundombinu.
“Mimi nasimamia miradi mikubwa ndani ya Halmashauri ya Bumbuli, iweje ni hujumu maji kwa wananchi wangu?” alihoji na kubainisha kuwa tayari wapo kwenye mchakato wa kuhakikisha vijiji vyote vinapata maji safi na salama kwa vipindi vitatu kwa wiki.
“Hiyo mikondo 72 wanayolalamikia kuwa inaenda kwa watu wengine kwa shughuli zao za kufyatulia matofali si kweli, kwa kawaida galoni (tenki) lililopo linazalisha lita 20,000 kwa kutwa na kupelekwa mara mbili kila kijiji, hivyo sasa ni wakati wa pamoja wananchi kujitokeza kusaidiana na si kulalamika na kuingiza ushabiki wa kisiasa,” alisema.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa