Home » » TBS yafungia viwanda

TBS yafungia viwanda

SHIRIKA la Viwango Tanzania {TBS} limefungia viwanda viwili mkoani hapa kwa tuhuma za kuzalisha bidhaa zilizo chini ya viwango.
Viwanda hivyo ni Akiis Bonny (Top Tang) kinachozalisha bidhaa za Tomato Sauce, Chilli Sauce na Bonny Cola, na kiwanda cha chumvi cha Hussein Salt Works.
Akifungia kampuni hizo, mkaguzi mkuu kutoka makao makuu ya TBS jijini Dar es Salaam, Hamisi Soudi alisema kuwa wamefungia uzalishaji bidhaa hizo baada ya kubainika kuwa hazijathibitishwa na shirika hilo la viwango.
“Tunafungia bidhaa hizi mpaka pale watakapoleta kwetu na kuzithibitisha kwa sababu huwezi kuwalisha watu bidhaa ambazo hazijathibitishwa,” alisema.
Soudi amewataka wakazi wa jiji la Tanga kuwa makini na bidhaa zinazozalishwa viwandani, kwamba zikiwa hazina lebo ya TBS wanapaswa kuacha kuzitumia kuepukana na matatizo yasiyo ya lazima.
Mwanasheria wa TBS, Baptister Bitaho alisema kuwa mzalishaji yeyote bila kujali ukubwa ama udogo wa  bidhaa anayozalisha, anatakiwa apate nembo ya TBS.
“Sisi  hatujali kama ni mzalishaji mdogo au mkubwa, lazima kila mmoja tumpatie nembo ya TBS kuthibitisha ubora wake,” alisema.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa