Home » » WMA WABAINI UDANGANYIFU KITUO CHA MAFUTA

WMA WABAINI UDANGANYIFU KITUO CHA MAFUTA

na Mwandishi wetu, Tanga
WAKALA wa Vipimo (WMA), wamebaini udanganyifu katika kituo cha mafuta cha WOCO wakati wakifunga pampu za vipimo sahihi vya kuuzia mafuta mjini Korogwe mkoani Tanga.
WMA ilifunga pampu mbili za petroli katika kituo hicho baada ya kubaini kuwa pampu hizo zilikuwa zikiwapunja wateja kwa wastani wa mililita 150 hadi 200 katika kila lita kumi.
Meneja wa WMA, Mkoa wa Tanga, Lucas Mosha, alisema walibaini udanganyifu huo hivi karibuni wakati wa ukaguzi wa kawaida ukiendelea ambao hufanya kila mwaka.
“Tuliwapa taarifa kwamba tunaenda kukagua pampu zao lakini siku tuliyofika hakukuwa na dizeli hivyo tukapima pampu za petroli tu, tulipofungua tukakuta ‘seal’ ya serikali imekatwa, jambo linaloashiria kuchezewa kwa pampu hizo ili ziweze kuwaibia wateja. Tulizifunga na kuwaamuru wasitumie pampu hizo hadi watakapopata maagizo mengine.
“Tulipoondoka tu, akaja mmiliki wa kile kituo akatoa zile lakiri tulizokuwa tumeweka na akaondoa tangazo huku akitoa vitisho na tulipoona hali hiyo, tuliamua kutoa taarifa polisi kwa ajili ya usalama,” alisema.
Mosha alisema tayari ameiarifu WMA Makao Makuu kwa hatua zaidi za kisheria dhidi ya mtu huyo kwani amekataa kukiri kosa na kutoa vitisho kwa watumishi wa mamlaka hiyo waliokuwa wakitekeleza wajibu wao.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa