Home » » SHIDA YA MAJI YAKWAMISHA MAENDELEO YA SHULE

SHIDA YA MAJI YAKWAMISHA MAENDELEO YA SHULE



Na Amina Omari, Muheza
WANAFUNZI wa Shule ya Sekondari Mbaramo wilayani Muheza, wamesema kuwa shule hiyo imeshuka kiwango cha taaluma kutokana na shida ya maji pamoja na uhaba wa vitabu vya kiada.

Hayo yalisemwa na wanafunzi hao wakati wakimweleza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, Ibrahimu Matovu, katika risala yao kwenye mahafali ya kuhitimu kidato cha nne yaliyofanyika jana shuleni hapo.

Jamali Bakari wa kidato cha nne akisoma risala hiyo, alisema kuwa shule hiyo inakabiliwa na shida ya maji na hivyo wanafunzi kutumia muda mwingi kutafuta maji badala ya kusoma.

Alisema kuwa tatizo jingine ni upungufu wa vifaa vya kufundishia , maktaba , maabara na usafiri hivyo wanafunzi wamekuwa wakisoma kwa tabu kutokana na wengi wao kuishi mbali na shule hiyo.

Wameiomba Serikali kuhakikisha wanatatua matatizo hayo kwa kuhakikisha vinapatikana vitu hivyo kwa kuwa ndiyo muhimu kwa misingi ya elimu bora.

Naye Mkuu wa Shule hiyo, Joseph Sakwela alisema kuwa matatizo hayo yameanza kushugulikiwa kutoka katika michango ya ada pamoja ya ujenzi wa shule hiyo na kwamba kuna baadhi ya mafanikio yamepatikana katika shule hiyo.

Akijibu Risala hiyo, Mkurungezi wa Wilaya ya Muheza, Ibrahimu Matovu alisema halmashauri ya wilaya hiyo itahakikisha inatatua tatizo la maji katika kipindi kifupi kijacho.

"Matatizo mengine tutaendelea kuyatatua kwa kiasi fedha zinavyopatikana, tutajaribu kumega fungu kidogo ili kuisaidia shule hiyo kwa nyakati tofauti licha ya ufinyu wa bajeti uliopo sasa," alisema Matovu.

Kwa upande mwingine kuhusu nidhamu aliwataka viongozi wa shule hiyo kukaa na wanafunzi hao ili kuwaelimisha kuhusu umuhimu wa elimu na tabia njema.

Chanzo: Mtanzania


0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa