Home » » WANAOTUPA TAKA HOVYO KUCHUKULIWA HATUA

WANAOTUPA TAKA HOVYO KUCHUKULIWA HATUA



Na Amina Omari, Korogwe
WATENDAJI wa Halmashauri ya Mji wa Korogwe wilayani hapa, wametakiwa kusimamia sheria ndogo ya kudhibiti uchafuzi wa mazingira na kuwachukulia hatua wanaotupa taka hovyo ili kuhakikisha mji huo unakuwa safi

Rai hiyo ilitolewa na Katibu Tawala wa Wilaya hiyo, Peter Mabuga, wakati wa kikao cha Kamati ya Ushauri ya Wilaya ya Korogwe (DCC), kilichofanyika juzi wilayani huo.

Alisema kuna udhaifu kwenye utekelezaji wa majukumu kwa baadhi ya watendaji wa halmashauri, jambo linalosababisha mji huo kuwa mchafu.

"Ifike mahali kila mtu atekeleze majukumu yake pasipo kusukumwa wala kuhimizwa, hasa suala la usafi, kwa nini sheria zimetungwa na Baraza la Madiwani halafu hazitumiki, ni lazima sheria hizo zitumike ili kuboresha mazingira ya mji huu kwa kuwalipisha faini wachafuzi wa mazingira," alisema Mabuga.

Naye Mkurungezi Halmashauri ya Korogwe Mjini, Lewis Kalinjuna alisema kwa sasa halimashauri hiyo imeanza kusimamia kwa ukaribu usafi wa mji huo katika maeneo ya katikati ya mji.

Alisema kinachofanyika sasa wananchi wanachangia Sh elfu moja kwa mwezi kwa ajili ya kuzolewa taka katika mitaa yao na trekta ambalo limenunuliwa kwa fedha za wananchi na halmashauri, huku wamiliki wakiwa ni wananchi.

Pia aliwataka viongozi kuwahimiza wananchi katika utunzaji wa mazingira na uchangiaji wa uhuduma ya usafi wa mji huo kwa maendeleo ya mji.

Chanzo: Mtanzania

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa