Home » » HIFADHI YA SAADANI YALALAMIKIWA

HIFADHI YA SAADANI YALALAMIKIWA

na Bertha Mwambela, Pangani
WAKAZI wa kijiji cha Saadani, kata ya Saadani, wilaya ya Pangani, mkoani Tanga, wameilalamikia Hifadhi ya Taifa ya Saadani kwa kushindwa kulipa fidia ya mali zao zilizoharibiwa mapema mwezi huu na wanyama aina ya tembo kijijini hapo.
Akizungumza na Tanzania Daima kwa niaba ya wanakijiji wenzake, Odongo Abielo, alisema kumekuwa na uharibifu mkubwa wa minazi zaidi ya 100 na nyumba 22 uliofanywa na tembo kwenye makazi na mashamba yao.
Alisema mbali na kupeleka taarifa kwenye ofisi za Hifadhi ya Taifa ya Saadani kuhusu uharibifu huo, hakuna hatua zozote zilizochukuliwa kwa ajili ya kuwalipa fidia.
“Tunasikitika sana kuhusu hii hifadhi yetu hapa kijijini, kwani haitusaidii tunapovamiwa na wanyama na kila tunapowafuata huwa hawachukui hatua yoyote,” alisema Abielo.
Kwa upande wake mkuu wa hifadhi hiyo, Hassan Nguluma, alikiri kuwepo kwa tatizo hilo na kusema kuwa suala la fidia ni jukumu la wizara na si la hifadhi kwani wao bado hawajapewa fungu kwa ajili ya matatizo ya fidia.
Alisema wao pamoja na hifadhi zote nchini, tayari walishapeleka malalamiko hayo kwenye wizara husika na kuwa swala hilo liko katika hatua za kushugulikiwa.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa