na Bertha Mwambela, Tanga
MFANYABIASHARA maarufu wa nafaka jijini Tanga, Mrisha Semvua (40), ameuawa kwa kupigwa risasi mbili kichwani na watu wasiojulikana.
Akizungumza na waandishi wa habari, Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Jafari Mohamedi, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo, majira ya saa moja jioni, nyumbani kwa marehemu maeneo ya Donge.
Alisema kuwa taarifa ya tukio hilo zilitolewa na majirani wa eneo hilo la Donge katika Kituo cha Polisi Chumbageni baada ya milio ya risasi kusikika.
“Baada ya milio ya risasi kusikika, majirani walitoka nje kushuhudia kilichotokea na kumkuta mfanyabiashara huyo akiwa amefariki dunia ndani ya gari, huku vioo vitatu vya gari lake vikiwa vimevunjwa, na kutoa taarifa polisi,” alisema kamanda huyo.
Alisema kuwa Jeshi la Polisi jijini hapa, linaendelea na uchunguzi ili kubaini chanzo cha tukio hilo pamoja na kuwakamata watuhumiwa ili kujibu tuhuma zitakazowakabili.
Chanzo: Tanzania Daima
0 comments:
Post a Comment