Home » » ORODHA YA VIWANDA VISIVYOFANYA KAZI NCHINI KUTOLEWA KESHOKUTWA

ORODHA YA VIWANDA VISIVYOFANYA KAZI NCHINI KUTOLEWA KESHOKUTWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Imeandikwa na Evance Ng’ingo
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage amesema hadi kufikia keshokutwa atakuwa ameshapewa orodha kamili ya viwanda vinavyotakiwa kunyang’anywa.
Kauli hiyo imekuja ikiwa ni siku moja baada ya Rais John Magufuli kuoneshwa kushangazwa na kukerwa na kitendo cha waziri huyo, kuchelea kuwanyang’anya umiliki wa viwanda wawekezaji walioshindwa kuviendeleza tangu walipobinafsishiwa miaka 20 iliyopita.
Dk Magufuli alitoa agizo hilo la kunyang’anywa kwa viwanda hivyo wakati akiwa kwenye ufunguzi wa kiwanda cha saruji cha Kilimanjaro, Kata ya Maweni jijini Tanga juzi. Kwa mujibu wa Rais Magufuli, nchi nzima ina viwanda 197 vilivyotelekezwa baada ya kubinafsishwa takribani miaka 20 iliyopita, vikiwemo viwanda vilivyopo mkoani Tanga. Kutokana na kauli hiyo ya Rais, Mwijage amesema hadi kufikia hiyo keshokutwa Alhamisi atakuwa ameshapata orodha kamili ya wanaotakiwa kunyang’anywa viwanda vyao, na siku inayofuata atayaweka wazi majina hayo.
Mwijage alisema makatibu wakuu wa wizara zote, ambazo kwa namna moja au nyingine zinahusika na viwanda, watakutana kuzungumzia wawekezaji huku pia wakuu wa mikoa wote nchini nao watashirikishwa. Alisema kwa kuwa yeye ni waziri anayeshughulikia viwanda, anatambua kuwa kuna viwanda ambavyo vipo chini ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi na wizara nyinginezo kwa hiyo ana wajibu wa kusikia kutokea wizara hizo.
Alibainisha kuwa kwa kuwa viwanda vingine vipo mikoani, ameona kuwa kuna haja ya kuwashirikisha wakuu wa mikoa kwa kuwa wao ndiyo wenyeviti wa Kamati za Ulinzi na Usalama wanaweza kumhakikishia viwanda vilivyoshindwa kuendelezwa na kama viliuzwa kweli kwa wawekezaji. Alisema kwa wawekezaji watakaonyang’anywa viwanda, hawatalipwa fidia ya aina yoyote ile kwa kuwa kwa miaka 20 wamepewa viwanda na wameshindwa kuviendeleza badala yake wamevitumia kama dhamana ya kuchukulia mikopo benki.
“Najua nimeshamuomba Rais kuwa asinikumbushe tena kwa kuwa kwanza nilishaambiwa kushughulikia suala hili na nikawa kidogo nalifuatilia kikawaida ila kwa sasa sina tena huo muda wa kuwabembeleza,” alieleza waziri huyo. “Kwa kawaida ukishindwa kumbwekea mtu utajikuta unabwekewa wewe na mimi nakwambia hiyo Ijumaa nitabweka ni kuwanyang’anya tu.”
Alifafanua kwamba wakati mwingine alikuwa akikwazwa na watu ambao wakati akiwaeleza kuhusu kuviendeleza, wakawa na visingizio vya kuwa na kesi mahakamani. Alisema Serikali ya Awamu ya Tano ilipoingia madarakani ilianza kuhimiza uanzishwaji wa viwanda na wapo Watanzania walioitikia kwa kuanzisha, lakini wamekuwa wakitumia gharama kubwa kununua maeneo na kuimarisha miundombinu ili hali wanaweza kupewa hivyo vilivyoshindwa kuendelezwa na mwekezaji na wakaviendeleza.
“Kuna mtu ana kiwanda Chalinze cha vigae amelazimika kuvuta maji kutokea mto Ruvu hadi Chalinze, kuvuta umeme takribani kilometa mbili kuelekea kwenye eneo la kiwanda chake, sasa mtu huyu anaingia gharama kubwa wakati watu kama hawa wakipewa kiwanda kilichotelekezwa na mwekezaji na kipo mazingira yenye miundombinu bora si anafanya kazi vema,” alieleza Mwijage.
Mbunge huyo wa Muleba Kaskazini mkoani Kagera, alisisitiza kuwa anaelewa kuwa Rais Magufuli bado ana imani naye na kuwa kama ni alama katika utendaji wake kwa wizara hiyo, anaweza kujipatia asilimia 60 ya uwezo kwa hiyo hatokubali mtu kumwangusha.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa