Home » » Wafugaji watozwa 3,000/- kwa kila ng’ombe

Wafugaji watozwa 3,000/- kwa kila ng’ombe

WAFUGAJI wilayani Kilindi, Tanga, wameitaka serikali kuwatendea haki sawa na wakulima katika kuchangia ujenzi wa maabara za shule za sekondari za kata.
Wakizungumza na Tanzania Daima jana, wafugaji hao walisema kitendo cha serikali kuwatoza sh 3,000 kwa kila ng’ombe mmoja kuchangia ujenzi huo si sahihi.
Walisema ni vema wakachangia kila kaya kama wanavyochangishwa wakulima.
Magu Kuhanga ni mmoja ya wafugaji wanaoishi Kijiji cha Kilindi, alisema michango hiyo imekuwa ikitozwa kwa nguvu na baadhi ya watendaji wa vijiji ambao wanawavizia ng’ombe wanapokwenda kunywa maji.
Alisema wanapofika katika kisima kilichopo katika Kitongoji cha Saibasi, Kijiji cha Negero, huwakamata wafugaji wasiolipa fedha hizo au wanalazimka kutoa ng’ombe mmoja kufidia fedha hizo.
Mfugaji Kidagari Mganya, mkazi wa Kijiji cha Mafisa, alisema   serikali kuwatoza wafugaji kwa kichwa kimoja cha ng’ombe kulipa fedha hizo ni kuwabagua kwa vile wao wanafuga ng’ombe.
“Huu ni ubaguzi kwa sababu wanatuonea sisi wafugaji, wakulima kila kaya wanachanga sh 10,000 kwanini tusiwe sawa na wenzetu, au kosa letu ni kuwa na ng’ombe?” alihoji Kidagari.
Alisema mifugo ni kama mazao mengine kwa kuwa inawafanya waishi kwa kuitegemea na kwamba kama wao wanatozwa fedha hizo kwa ng’ombe mmoja basi serikali ingewatoza wakulima sh 3,000 kwa kila gunia moja la mkulima alilopata shambani ili wawe sawa.
Kidagari alisema kutokana na michango hiyo kuwekwa wafugaji watalazimika kuchangishwa fedha nyingi kutokana na kwamba mtu mmoja anaweza kumiliki zaidi ya ng’ombe 100.
Mkuu wa Wilaya, Selemani Liwowa, alipoulizwa kuhusu suala hilo alikiri kuwepo kwa michango hiyo lakini akasema wamepanga kutoza kila ng’ombe mmoja sh 2,000 na wala si sh 3,000.
“Ni kweli tunawatoza wafugaji sh 2,000 na wala si sh 3,000 waliyosema na mpango huu tumeubuni kutokana na pato la mtu alilonalo, sasa tumepanga kila mwenye ng’ombe atalipa sh 2,000 kwa ng’ombe mmoja, kondoo na mbuzi mmiliki wake atalazimika kulipa sh 500 kwa mnyama mmoja,” alisema Liwowa.
Mkuu huyo wa wilaya alisema michango hiyo wameiweka kulingana na kipato cha mtu, akatoa mfano kuwa yeye kama mkuu wa wilaya amelazimika kuchangia ujenzi huo kwa kutoa sh 500,000 kutoka katika mshahara wake.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa