Home » » Serikali sasa yaombwa kupunguza pembejeo

Serikali sasa yaombwa kupunguza pembejeo

Lushoto. Wakulima wa Kilimo cha Mbogamboga na Matunda wilayani Lushoto, mkoani Tanga, wameomba Serikali kuwapunguzia gharama za pembejeo za kilimo ili walime kisasa.
Wakizungumza kwenye kikao cha  Umoja wa Wakulima wa Mbogamboga na Matunda Wilaya ya Lushoto na Korogwe ulioitishwa na  Shirika la Oxfam Tanzania tawi la Lushoto juzi, wakulima hao walisema kwa kipindi kirefu wameomba Serikali kupunguza gharama bila ya mafanikio.
Walisema hali hiyo imekuwa ikirudisha nyuma jitihada zao, badala yake kulima kwa mazoea jambo ambalo linawafanya wengi kutokuona faida ya kilimo.
“Tumekuwa tukikutana na kutoa kero zetu bila kupatiwa ufumbuzi,  hutujui tuwasilishe vipi ili Serikali itusikilize... tumekuwa tukipoteza muda wetu kila siku,” alisema Juma Dhahabu  na kuongeza:
“Oxfam kwa upande wenu tunawashukuru kwa kutupatia msaada mdogomdogo na kutukutanisha na wataalamu wa kilimo na wadau wake.”  Dhahabu alisema ni jambo la kushangaza kuona mkulima wa Lushoto akiwa maskini ilhali wilaya hiyo ina rutuba inayofaa  kwa aina tofauti  za  kilimo, ikiwamo kilimo cha njegere, hivyo kuitaka Serikali kuwaunga mkono hasa pembejeo
Naye Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya  Lushoto, Jumanne Shauri alitaka Oxfam kutoa elimu kwa wakulima kuhusu kilimo cha mbogamboga na matunda, kwa sababu wengi hawana elimu hiyo.
Shauri alisema baadhi ya wakulima hawana elimu hivyo kushindwa kulima kilimo chenye tija.  Alisema iwapo mkulima wa njegere atapatiwa elimu stahiki,  ni wazi wakazi wengi wa Lushoto na Korogwe watakimbilia kilimo hicho.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa