Home » » Tiketi za elektroniki zafeli Tanga

Tiketi za elektroniki zafeli Tanga

MASHABIKI wa soka mkoani Tanga, wameliomba Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kutoa elimu kuhusiana na mfumo mpya wa tiketi unaotolewa kwa njia ya kieletroniki kwani umewaleta adha.
Wakizungumza jijini hapa juzi, walisema kuwa hawapingi kuwepo na mfumo huo, bali hakukuwa na maandalizi kwa kutoa elimu kwa mashabiki, hivyo wanaona kama shirikisho hilo limekurupuka na kushauri bora ungeanza mwakani na muda huu wautumie kuelimisha kuhusiana na matumizi ya mfumo huo.
Mmoja wa mashabiki hao, Athumani Mnyamisi, alisema kuwa shirikisho hilo limekurupuka, hivyo ni bora wangeacha hadi mwakani, hivyo kipindi hiki wakitumie kuelimisha wadau au mashabiki wa soka ili waweze kuwa na uelewa utakaofanya kusitokee mgogoro.
“Mfumo huu mi naona kama wamekurupuka, kwa sababu sisi mashabiki hatuna uelewa na hili jambo, kwani tumefika uwanjani toka saa nane milango ni miwili tu inatumika, mpaka saa kumi na nusu mpira umeanza bado hatujaingia uwanjani,” alisema.
Shabiki mwingine, Salimu Abdallah, aliupongeza mfumo huo kuwa unapunguza ubadhirifu wa fedha ila bado mashabiki wengi wa soka hawana uelewa nao, hivyo itachukua muda kuweza kufahamika na kutumika bila vikwazo hapa nchini.
Hata hivyo, Meneja wa Uwanja wa Mkwakwani, Mbwana Msumari, alisema kuwa tatizo mashabiki wa soka hawana uelewa na mfumo huo, hivyo kulazimika kutumia mfumo wa zamani wa kuuza tiketi kwa kawaida.
“Nimenusurika kupigwa na mashabiki kutokana na kushindwa kuuelewa mfumo huu na bei ya tiketi kupanda, badala ya elfu tatu kwa mechi imekuwa elfu tano, hivyo tukalazimika kuuza tiketi kwa mfumo wa zamani ili mashabiki waweze kuingia na kutazama mpira,” alisema Msumari.
Katika mechi hiyo, wenyeji Coastal Union walipata bao dakika ya kwanza likifungwa na Yayo Lutumba huku JKT Oljoro kutoka Arusha wakisawazisha dakika ya 87 kwa bao la Amisi Salehe.  
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa