Home » » Mbaroni kwa kukutwa na bunduki, sare za polisi

Mbaroni kwa kukutwa na bunduki, sare za polisi

JESHI la Polisi Mkoa wa Tanga linawashikilia watu watano kwa tuhuma za kukutwa na bunduki aina ya Shotgun na sare za Jeshi la Polisi ambazo zilitumika katika matukio ya uhalifu wilayani Korogwe.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Constantine Massawe, alisema jana kuwa watuhumiwa hao walikamatwa Desemba 28 mwaka jana, saa 4 usiku katika eneo la Kambi ya Mkonge ya Gomba, Kata ya Makuyuni, Tarafa ya Mombo.
Alisema watuhumiwa hao walikuwa wakiitumia bunduki hiyo yenye namba za usajili 807028 ikiwa na risasi tatu na ganda moja katika kufanyia uhalifu katika maeneo mbalimbali.
Aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Zakaria Jelas (50), Moses Jonas (44), Selemani Hassan (21), Taratibu Hemed (74) na Hemed Taratibu (32), wote wakazi wa Makanya, wilayani Same, Kilimanjaro.
Kamanda Massawe alisema baada ya upekuzi watuhumiwa hao walikamatwa na sare mbili mali ya Jeshi la Polisi Tanzania zikiwemo shati mbili za polisi na suruali ambayo waliikata kama kaptula na kwamba walipohojiwa walikiri kuhusika na matukio mbalimbali ya unyang’anyi na utekaji wa magari.
Katika tukio jingine, Jeshi la Polisi mkoani Tanga linawashikilia wakazi watatu kwa tuhuma za  kupatikana na mali inayodhaniwa kuwa ni  ya wizi.
Watu hao walikamatwa juzi, saa 6 mchana katika kizuizi cha Polisi kilichopo Kijiji Kwasunga, Kata ya Makuyuni, Tarafa ya Mombo, wilayani Korogwe wakiwa na pikipiki mbili za wizi ambazo ziliibiwa Kariakoo, Dar es Salaam.
Aliwataja waliokamatwa kuwa ni Jackson Aloyce (25) na Leonard Frederick (21) wakiwa na pikipiki yenye namba za usajili T 274 CQV Boxer rangi ya bluu na Karist Adolf (22) akiwa na pikipiki T 162 CKL Boxer, rangi nyeusi.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa