Home » » Jela miaka 30 kwa kupora bodaboda

Jela miaka 30 kwa kupora bodaboda

na Mohammed Mhina, Handeni
 
MAHAKAMA ya Wilaya ya Handeni, mkoani Tanga, imemhukumu kifungo cha miaka 30 jela mkazi wa Kijiji cha Kibirashi, Ramadhani Samselo (20) baada ya kupatikana na hatia ya kupora pikikipiki (bodaboda) kwa kutumia silaha.

Akitoa hukumu hiyo jana mbele ya umati uliokuwa umefurika mahakamani hapo wakiwamo waendesha bodaboda wa wilaya za Kilindi na Handeni, Hakimu Maligana, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama hiyo, Patrick Maligana, alisema ameridhishwa na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka, hivyo kumtia hatiani mtuhumiwa bila shaka kwa kosa aliloshitakiwa nalo.

Alisema anatoa hukumu hiyo ili iwe fundisho kwa wengine wanaowania mali za watu wengine wakati wakitafuta kipato halali.
Alipotakiwa kujitetea kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo, mshitakiwa alieleza kuwa anaiachia mahakama itoe adhabu inayomfaa.

Awali, Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Nzagalila Kikwelele, alidai Januari 29 mwaka huu, majira ya saa 2:00 usiku mwaka huu huko Kibirashi, Samselo akijifanya ni msafiri na kukodi pikipiki (bodaboda) ya Mngoya Kigono, ili impeleke nyumbani kwake.

Alidai wakiwa njiani mtuhumiwa Samselo alianza kumshambulia mwendesha bodaboda huyo kwa kisu sehemu ya mbavuni na mikononi na baadaye kuanguka chini na kumpora pikipiki hiyo T. 959 AXN Sunlag.

Alidai baada ya mtuhumiwa kuondoka eneo la tukio, mlalamikaji alimpigia simu mmoja wa waendesha bodaboda mwenzake na ndipo walitoka kwa wingi kumfuatilia na kumkuta akiwa amelala chini huku akitokwa na damu nyingi ambapo walimchukua kumpeleka hospitalini huku wengine wakimfuatilia mtuhumiwa.

Alidai vijana hao walipofika mbele kidogo walimkuta mtuhumiwa akiongeza mafuta lakini alitimua mbio na kuiacha pikipiki hiyo baada ya kubaini alikuwa akifuatiliwa.

Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa