Home » » Wamzuia mbunge waeleze kero

Wamzuia mbunge waeleze kero

WANANCHI wa Kijiji cha Kwefingo kilichopo Kata ya Dindira, wilayani Korogwe, walizuia msafara wa Mbunge wa Korogwe Vijijini, Stephen Ngonyani ‘Profesa Majimarefu’, ili waweze kumweleza kero zao.
Wananchi hao waliokuwa na mabango yenye ujumbe mbalimbali, walimsimamisha mbunge huyo baada ya kumaliza mkutano wa hadhara katika kijiji hicho.
Akiwasilisha kero hiyo mbele ya mbunge huyo, Ismail Bendera, alisema wanashangaa kuona nguzo za umeme zikiwekwa katika Kijiji jirani cha Mgwashi badala ya umeme huo kuanza kufika katika kijiji chao ambacho ndipo makao makuu ya kata hiyo.
“Tunashangaa tumewahi kukusikia bungeni ukitaja kwamba umeme utakuja hapa katika kijiji chetu, lakini mbona sasa tunaouna umekwenda katika kijiji ambacho anatoka diwani?” alihoji Bendera.
Mkazi mwingine, Bakari Kibwana, alisema wamesikia taarifa kwamba umeme hautafika katika kijiji chao na kwamba endapo suala hilo litakuwa kweli watakuwa tayari kufunga ofisi za kata ili kushinikiza umeme ufike katika kijiji chao.
Akijibu maswali hayo, mbunge huyo alisema suala la umeme huo ambao ni mpango wa serikali wa usambazaji wa umeme vijijini (REA), katika jimbo lake utasambazwa katika vijiji kumi kijiji chao kikiwemo.
Aliwatajia vijiji hivyo kata zake zikiwa kwenye mabano kuwa ni Kwefingo (Dindira), Mgobe na Gereza (Makuyuni), Mkwakwani na Kwemzindawa (Mnyuzi), Lusanga na Makumba (Kerenge), Alamisi, Matalawanda na Kijango (Magoma) na Kijiji cha Vugiri kilichopo Kata ya Vugiri.
Hata hivyo aliwahakikishia umeme utafika katika kijiji hicho na kwamba atafuatilia kujua namna watakavyoufikisha katika kijiji hicho.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa