Home » » SIKU 160 ZA MIUJIZA NEC

SIKU 160 ZA MIUJIZA NEC

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Rais Jakaya Kikwete.
Wakati bado ikielemewa na majukumu mazito matano, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) imezidi kujiongezea mzigo mwingine zaidi, ambayo utekelezaji wake hadi kukamilika ndani ya siku 160 kabla ya kufanyika uchaguzi mkuu Oktoba 25, mwaka huu kuwa miujiza.
 
MGAWANYO WA MAJIMBO
Nec imejiongezea jukumu lingine zito ambalo ni la sita baada ya kutangaza kuanza mchakato wa kuchunguza mipaka na kugawa majimbo kwa ajili ya uchaguzi huo, huku ikitaja tarehe ya mwisho ya kuwasilisha maombi kwa wadau wenye nia ya kugawa jimbo/majimbo yanayokidhi vigezo kuwa ni Mei 31, mwaka huu.
 
Mchakato huo ulitangazwa kupitia taarifa ya Nec iliyochapishwa kwenye vyombo vya habari juzi iliyosainiwa na Mkurugenzi wa Uchaguzi, R.K. Kairima. 
 
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, uamuzi wa Nec wa kujiongezea jukumu hilo umezingatia Ibara ya 74 (6) (c) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya mwaka 1977, ambayo inaipa tume hiyo mamlaka ya kuchunguza mipaka na kugawa maeneo kwa ajili ya uchaguzi wa wabunge.
 
Pia umezingatia Ibara ya 75 (4) ya katiba hiyo, inayoipa Nec uwezo wa kugawa majimbo mara kwa mara na angalau kila baada ya miaka 10.
 
“Hivyo, Tume inakusudia kuanza mchakato wa kuchunguza mipaka na kugawa majimbo kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
 
Miongoni mwa vigezo vitakavyotumika katika kuchunguza mipaka na kugawa majimbo ni pamoja na mgawanyo wa wastani wa idadi ya watu katika jimbo inayopatikana kwa kuchukua idadi ya watu wote nchi nzima na kugawanywa kwa idadi ya majimbo yaliyopo.
 
Vigezo vingine ni idadi ya watu iliyotokana na makisio ya ongezeko la watu hadi Julai, mwaka huu na kwamba, majimbo yenye watu wengi yatafikiriwa zaidi; pia upatikanaji wa mawasiliano, hali ya kijiografia, kiuchumi, ukubwa wa eneo la jimbo husika na mipaka ya kiutawala.
 
Vingine ni jimbo moja kutokuwa ndani ya wilaya/halmashauri mbili, kata moja kutokuwa ndani ya majimbo mawili, mpangilio wa maeneo ya makazi ya watu yaliyopo, mazingira ya Muungano, uwezo wa ukumbi wa Bunge na viti maalumu vya wanawake.  
 
Utaratibu utakaofuatwa kuwasilisha maombi umetajwa kuwa ni maombi/mapendekezo ya kugawa majimbo au kurekebisha mipaka kuwasilishwa kwa mkurugenzi wa halmashauri husika, ambayo yatajadiliwa katika vikao rasmi.
 
“Inashauriwa vikao hivyo vishirikishe wadau mbalimbali,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo.
 
Pia mkurugenzi wa halmashauri atawasilisha maombi/mapendekezo kwa Katibu Tawala (RAS), Katibu Tawala Mkoa atayawasilisha katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) ili kupata maoni zaidi na katibu huyo atawasilisha mapendekezo Nec.
 
Taarifa hiyo imewataka wadau wote wenye nia ya kugawa jimbo/majimbo yanayokidhi vigezo hizo kuwasilisha maombi yao Nec kwa kufuata utaratibu huo.
 
Hata hivyo, taarifa hiyo ilieleza kuwa maombi yote yaliyo chini ya mgawanyo wa wastani wa idadi ya watu hayatafanyiwa kazi.
 
 
ZABUNI VIFAA VYA UCHAGUZI.
Nec pia imeanzisha mchakato wa zabuni ya vifaa vinavyohitajika kwa ajili ya uchaguzi kwa kutoa siku 60 kwa miongozo ya  vitu 23 vinavyohitaji kuombewa zabuni na wazabuni.
 
Kwa mujibu wa tangazo lillitolewa na Nec katika Gazeti la Daily News la Mei 14, mwaka huu zabuni hizo zilitangazwa na tume hiyo Mei 13, mwaka huu.
 
Tangazo hilo limeelekeza kuwa Nec itafunga upokeaji wa maombi ya wazabuni watakaotaka kutoa huduma na vitu vilivyoorodheshwa Mei 16, mwaka huu.
 
Katika tangazo hilo, zabuni hizo zitaanza kutolewa Mei 23 kwa wazabuni ambao watakuwa tayari wamehakikiwa Mei 17, mwaka huu. 
 
Zabuni zilizotangazwa na Nec kwa ajili kuombwa  ni pamoja na usambazaji wa fulana, kofia, mikoba ya waangalizi wa uchaguzi, kuchapisha na kusambaza karatasi za uchaguzi,  usambazaji wa wino wa kupigia kura, usambazaji wa vifaa vya uchaguzi na mabetri.
 
Baadhi ya vitu na huduma zilizotangazwa kuombewa zabuni, ni usambazaji wa vifungio vya makasha ya kupigia kura, magurudumu, mafuta ya dizeli, kompyuta mpakato, mashine za kuchapisha karatasi, magari, huduma za  usafiri wa ndege, huduma za marekebisho ya tovuti ya Nec.
 
Nyingine ni utoaji wa tiketi za ndege, sehemu za kufanyia mikutano, malazi, dawa za kupulizia kuua wadudu, chakula na vinywaji, ulinzi na vifaa vya kujikinga na moto, usambazaji wa vifaa vya kompyuta, usambazaji wa vifaa vya kutolea elimu kwa wapiga kura, vifaa vya kujikinga pamoja na vifaa vya kufanyia usafi.
 
DAFTARI BVR.
Wakati ikijiongezea majukuku mengine,  hadi sasa Nec bado inaelemewa na majukumu mengine matano, likiwamo linalohusu uandikishaji wananchi katika daftari la kudumu la wapigakura kwa kutumia mfumo mpya wa Biometric Voters Registration (BVR).
 
Uandikishaji huo, ambao umekuwa ukisuasua tangu kuanza kwake Februari 23, mwaka huu katika mkoa wa Njombe na hivyo, kusababisha kukwama kwa kura ya maoni iliyokuwa imetangazwa na Rais Jakaya Kikwete kuwa ingefanyika Aprili 30, mwaka huu.
 
Uandikishaji katika Mkoa wa Njombe ulikamilika katikati ya Aprili.
 
Hadi sasa mchakato, ambao umekwishakamilika katika mkoa huo pekee, unaendelea katika mikoa ya Ruvuma, Lindi, Mtwara na Iringa.
 
Awali, Nec ilitangaza kuwa uandikishaji katika mikoa ya Mbeya, Dodoma, Tabora na Katavi ungeanza Mei 2, mwaka huu, lakini kwa sababu zizizojulikana haujaanza huku Nec ikiahidi kuwa utaanza kesho.
 
KAMPENI
Jukumu lingine zito linaloikaba koo Nec ni maandalizi ya kampeni za uchaguzi mkuu ambazo kisheria zinatakiwa kuchukua siku 72.
 
UCHAGUZI MKUU
Baada ya kampenni za uchaguzi, Nec itakabiliwa na jukumu la kusimamia na kuratibu upigaji kura za udiwani, ubunge na urais utakaofanyika Oktoba 25, mwaka huu sambamba na kutangaza matokeo.
 
 
KURA YA MAONI
Hadi sasa haijajulikana ni lini kura ya Katiba inayopendekezwa itafanyika.
 
Awali, Nec ilitangaza kwua ingefanyika Aprili 30, lakini ilishindikana kutokana na kutokukamilika kwa Daftari la Kudumu la Wapigakura.
 
Kufuatia ahli hiyo, Nec ilitangaza kuwa itakamilisha Daftari kabla ya julai, mwaka huu na kwamba suala la tarehe ya kura ya maoni litafuata, baada ya kushauriana na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (Zec).
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa