Home » » MWILI WA JAJI MAKAME KUZIKWA TANGA

MWILI WA JAJI MAKAME KUZIKWA TANGA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Familia ya Jaji Lewis Makame imesema haitasahau namna jaji huyo alivyoijali na kulitumikia taifa kwa uaminifu hadi mauti yalipomfika juzi mchana.
Akizungumzia utaratibu wa maziko ya kiongozi huyo jana, mwanaye Eugene alisema kutokana na mchango wake mkubwa kwa familia na kwa taifa, watatumia siku nne ili kutoa fursa kwa familia na viongozi wa ngazi mbalimbali nchini kutoa heshima zao za mwisho.
Alisema kwa sasa familia inaendelea kuratibu na kusimamia utaratibu wa awali wa maziko yake yanayotarajiwa kufanyika katika Kijiji cha Tongwe Muheza, mkoani Tanga ambako alizaliwa.
“Hadi sasa tunaendelea na maandalizi ya maziko ya mzee wetu na ibada maalumu ya kumuaga itafanyika hapa nyumbani siku ya Ijumaa asubuhi kabla ya kuelekea Kanisa la St Alban na baadaye tutampeleka katika Kijiji cha Tongwe kwa ajili ya kuupumzisha mwili wake kwa amani,” alisema Eugene.
Alisema baba yake alifariki dunia juzi saa 7.45 mchana katika Hospitali ya AMI Trauma, Masaki, alikokuwa amelazwa kwa takriban mwezi mmoja.
Wakati huohuo, Rais Jakaya Kikwete amemtuma salamu za rambirambi kwa mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) na familia ya marehemu kutokana na kifo hicho.
Taarifa iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Ikulu, ilisema Rais amepokea taarifa za kifo hicho kwa masikitiko, kwa kuwa ni miongoni mwa watu waliolitumikia Taifa kwa uaminifu, uadilifu, bidii na umahiri mkubwa.
Rais Kikwete alisema uongozi wake ulichangia kuimarisha amani, utulivu, umoja na mshikamano wa kitaifa katika mazingira mapya ya demokrasia ya vyama vingi vya siasa hapa nchini.
Chadema watoa salamu
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), nacho kimetuma salamu za rambirambi na kusema kuna haja ya kupongeza utumishi wake katika kipindi chote alichokuwa akilitumikia Taifa akiwa mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa