Home » » MILIONI 270 WAHUSIKA AJALI ZA KEMIKALI

MILIONI 270 WAHUSIKA AJALI ZA KEMIKALI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
INAKADIRIWA kuwa watu milioni 270 wanahusika na ajali za kemikali maeneo ya kazi, huku milioni 160 wanasumbuliwa na magonjwa yatokanayo na athari za kemikali kila mwaka kati ya watu bilioni 2.8 wanaofanya kazi duniani kote.
Takwimu hizo ni kwa mujibu ya Shirika la Kazi Duniani (ILO) zilizotolewa na Mkemia Mkuu wa Serikali, Profesa Samweli Manyele wakati akifungua mafunzo ya wadau juu ya usalama wa kemikali bandarini na wakati wa usafirishaji iliyofanyika mkoani hapa jana.
Alisema kutokana na takwimu hizo, Serikali ya Tanzania ipo kwenye mkakati wa kuchukua hatua ikiwemo kutoa mafunzo kwa wasafirishaji ili kuhakikisha wanapunguza athari zinazosababishwa na kemikali za viwandani.
“Nchi yetu ina matumizi makubwa ya kemikali aina ya Ammonium Nitrate ambayo ina asili ya kulipuka, na inatumika kwenye mbolea ili kuongeza uzalishaji na kemikali nyingine zenye athari zinazotumika kwenye viwanda.
“Ipo haja ya makusudi kuhakikisha usafirishaji wake hauleti athari kwa binadamu na viumbe wengine,” alisema Profesa Manyele na kuongeza kwamba baadhi ya matukio yaliyo nje ya utaratibu ulioruhusiwa wa tindikali yamesababisha athari kwa watu tisa kwenye mikoa ya Dar es Salaam, Mwanza na Zanzibar mwaka 2013.
Alisema mwaka huu ilihusisha matukio ya ajali za magari kupinduka wakati wa usafirishaji tindikali maeneo ya Morogoro na Dar es Salaam ambapo ilidhibitiwa hivyo haikuleta athari.
Profesa Manyele alisema katika kudhibiti athari za kemikali, serikali kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imeanza mchakato wa kuwa na kituo cha kuratibu na kudhibiti athari za sumu ili kutoa msaada wa haraka katika matukio ya sumu na ajali zinapotokea.
“Mpaka Julai mwaka huu tutakuwa tumetoa kanuni mpya ambazo zimeboreshwa kwa kiasi kikubwa ili kulinda eneo la usafirishaji na makampuni yanayojihusisha na usafirishaji wa kemikali hizo kuwa salama,” aliongeza mkemia huyo.
Mkurungezi wa Usimamizi na Udhibiti wa Kemikali, Sabanitho Ntega, alisema mafunzo hayo yamewalenga wafanyakazi wa bandarini kwani ndio lango kuu la kupitisha kemikali kutoka nje ya nchi kwa ajili ya matumizi ya viwanda.
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa