Home » » Pangani Wapata Kivuko Kipya

Pangani Wapata Kivuko Kipya

Wananchi wa Pangani/Bweni mkoani Tanga wamepata kivuko kipya cha MV. Tanga, ambacho sasa kitasaidiana na MV. Pangani II kutoa huduma katika eneo la Pangani/Bweni.
MV. Tanga iliwasili Pangani siku ya ijumaa saa moja jioni, ikitokea katika bandari ya Dar es salaam ambako ndiko ujenzi wake ulifanyika. Ujenzi wa kivuko cha MV. Tanga umefanywa na Kampuni ya kitanzania iitwayo Songoro Marine Company Ltd.
Akiongea na wananchi wa Pangani Naibu Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi kutoka Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Lazaro Vazuri  alisema kuwa kukamilika kwa ujenzi wa kivuko kipya cha MV. Tanga ni muendelezo wa sera ya Serikali ya kuboresha huduma kwa wananchi wake.
Nae Mtendaji Mkuu TEMESA Mhandisi Lekujan Manase alisema “TEMESA imejipanga kuhakikisha kuwa vivuko vyake vyote vinafanyiwa matengenezo ya kinga kwa wakati, ili kuhakikisha kuwa huduma kwa wananchi wanaotumia vivuko hivyo inapatikana kwa wakati muafaka hivyo MV. Pangani II sasa itakwenda kwenye ukarabati na baada ya ukarabati huo vivuko vyote viwili vitabakia katika eneo la Pangani/Bweni ili kuendelea kutoa huduma kwa wananchi.”
Wananchi wa Pangani/Bweni wamekipokea kivuko cha MV. Tanga kwa furaha kubwa na kuiomba Serikali kutoa huduma ya kivuko kwa saa 24  kwa siku ili kuwasaidia wananchi hasa wa eneo la Bweni kupata huduma hiyo nyakati za usiku wanapohitaji kupata huduma za kijamii upande wa Pangani.
MV. Tanga ina uwezo wa kubeba tani 50 ambazo ni sawa na kubeba abiria 100 na magari 6 kwa pamoja. Uwezo wa MV. Tanga unalingana na uwezo wa kivuko cha MV. Pangani II.

Imetolewa na,
 Kitengo cha Habari na Mawasiliano TEMESA

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa