Home » » Kibali chasubiriwa ukarabati mtandao wa majitaka uanze

Kibali chasubiriwa ukarabati mtandao wa majitaka uanze

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Tanga (Uwasa) imesema inasubiri kupata kibali cha dharura kutoka kwa Wakala wa Manunuzi wa Serikali (GPSA) kukarabati mtandao wa majitaka katika baadhi ya maeneo ambayo yanahatarisha afya za wakazi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Tanga- Uwasa, Joshua Mgeyekwa amebainisha hayo jana katika taarifa yake kwa vyombo vya habari kuhusu mchakato wa uzibuaji wa mtandao wa majitaka katika maeneo mbalimbali ya jiji na kusema lengo ni kutatua changamoto hiyo.
Aliyataja maeneo yatakayohusika na ukarabati kuwa ni Usagara, barabara ya Swahili pamoja na barabara za 11, 12, 13 na 14 Lumumba ambayo mabomba yake ya kupitisha majitaka yamevunjika kutokana na mvua za masika zinazoendelea kunyesha msimu huu.
“Mvua zinazoendelea kunyesha zimefanya udongo uelemee mabomba ambayo yamechakaa kutokana na asili ya kemikali zilizomo kwenye majitaka …na kwakuwa yametengenezwa kwa ‘Asbestos’ kumefanya mabomba husika kuvunjika na kuziba hatua ambayo inazuia majitaka kutiririka vizuri na badala yake huzagaa mtaani na kuhatarisha afya za wakazi. Ili kupata ufumbuzi wa tatizo hili tayari mamlaka imeomba kibali cha manunuzi ya dharura kwa wakala wa manunuzi GPSA kwa ajili ya kupata mkandarasi mwenye mitambo ili kwa haraka afanye ukarabati huo ambao tunaamini utarejesha mfumo katika hali ya kawaida”, alisema.
Aidha, aliwataka wananchi kuwa wavumilivu kwa kuchukua tahadhari zinazostahili hasa wakati huu ambapo Uwasa inafanya udhibiti wa muda wa majitaka.

Chanzo Gazeti la Habari leo
 

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa