MAMEYA na Wenyeviti wanaounda Umoja wa Katiba ya wananchi (Ukawa)
ambao walihudhuria mkutano mkuu maalum wa uchaguzi wa Umoja wa Serikali
za mitaa wametishia kujitoa katika umoja huo kwa sababu ya kukiukwa
taratibu mbalimbali.
Msimamo huo waliutoa Dodoma jana saa chache baada ya kususia
mkutano huo wakipinga majina ya wagombea wao kukatwa bila kuelezwa
sababu za msingi.
Katika taarifa yao jana, walitoa orodha ndefu ya kukiukwa
taratibu hizo ikiwa ni pamoja na hatua ya ALAT kumruhusu waliyemuita
‘meya batili’ wa jiji la Tanga kuhudhuria na kugombea nafasi ya makamu
mwenyekiti wa Jumuiya hiyo.
Mameya hao na wenyeviti wa Ukawa walisema; “Machapisho ya ALAT
tuliyopewa ukumbini yalikuwa na picha za wajumbe waliovaa sare za Chama
Cha Mapinduzi (CCM) wakati ALAT ni chombo kisichofungamana na chama
chochote cha siasa. Mfano Meya wa Manispaa ya Dodoma anaonekana kwenye
kabrasha la ratiba akiwa amevalia sare za CCM.
“Katibu mkuu kutokuchapisha orodha ya wagombea na kuisambaza kwa
wajumbe wa mkutano huo kwa mujibu wa kifungu cha 30 (6) cha kanuni za
kudumu za mkutano na uchaguzi wa viongozi wa jumuiya za serikali za
Mitaa za mwaka 2009”.
Mwenyekiti ALAT apatikana
Wakati huohuo, ALAT jana ilipata mwenyekiti mpya licha ya wajumbe kutoka Ukawa, wakisusia uchaguzi huo kwa kutoka nje ya ukumbi.
Wajumbe walimchagua Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Gulam Mukadam
kuwa mwenyekiti wa jumuiya hiyo kwa kura 179 kati ya kura 281
zilizopigwa.
Mgombea mwingine katika nafasi hiyo alikuwa ni Murshid Ngeze aliyepata kura 97 huku kura tano zikiharibika.
Huo ni mkutano wa kwanza wa jumuiya hiyo katika uongozi wa Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dk. John Magufuli.
Awali, Mwanasheria wa ALAT, Cleofasi Manyangu, alisema nafasi
zilizokuwa zikigombewa ni mwenyekiti, makamu mwenyekiti na nafasi za
wajumbe wa kamati ya utendaji.
“Wakati wa mchakato wa uchaguzi huu waliochukua na kurejesha fomu za
kugombea uenyekiti wa ALAT ni Gulam Mukadam, Murshid Ngeze ambaye ni
Meya wa Bukoba Vijijini, Chifu Kalumuna ambaye ni Meya wa Bukoba Mjini
na Isaya Mwita ambaye ni Meya wa Jiji la Dar es Salaam.
“Waliokidhi vigezo kwa mujibu wa Katiba ya ALAT ni watia nia wawili
ambao ni Mukadam na Ngeze na waliosalia hawakukidhi vigezo vya kuwa
wagombea.
“Vigezo hivyo vilikuwa ni kurejesha fomu katika muda usiozidi saa
6:00 ya siku moja kabla ya uchaguzi na pia wagombea hao hawakupata
wadhamini 10 kama taratibu zinavyoelekeza,” alisema Manyangu.
Wakati Manyangu akisema hayo, Mwenyekiti wa muda wa mkutano huo
ambaye pia ni Meya wa Dodoma, Jafari Mwanyemba, alitangaza rasmi kwamba
watakaogombea katika uchaguzi huo ni Mukadam na Ngeze jambo
lililosababisha wajumbe wa Ukawa kususia shughuli zote za uchaguzi huo.
CHANZO: MTANZANIA.
0 comments:
Post a Comment