Home » » WAFUGAJI WA NG'OMBE WAPEWA MILIONI 230/-

WAFUGAJI WA NG'OMBE WAPEWA MILIONI 230/-

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
MRADI wa kusambaza mitambo ya bayogesi ngazi ya kaya nchini (TDBP), umetoa Euro 100,000 (Sh milioni 230) kwa Chama Kikuu cha Ushirika cha Wafugaji Ng’ombe wa Maziwa cha Mkoa wa Tanga (TDCU).
Mratibu wa TDBP, Lehada Shila amesema fedha hizo, zitatumika kutengeneza mfuko wa mzunguko wa kutoa mikopo ya masharti nafuu ili kuwawezesha wanachama wa TDCU wakope na kununulia mitambo ya bayogesi inayoratibiwa na TDBP.
Alisema hayo katika sherehe za kuzindua awamu ya pili ya mradi huo, zilizofanyika Kijiji cha Boza Wilaya ya Pangani mkoani Tanga hivi karibuni, ”Kwa kujua umuhimu wa mitambo ya bayogesi katika kuleta mapinduzi ya kilimo na viwango vya maisha miongoni mwa wakulima nchini, Serikali za Tanzania na Norway kupitia Wakala wa Nishati Vijijini umetoa fedha za kuwapatia punguzo la bei ya mitambo ya bayogesi la takribani Sh 240,000 kwa kila mtambo unaolipiwa na mkulima, hivyo kumfanya alipe Sh 960,000 tu badala ya bei ya awali ya Sh milioni 1.2,” alieleza Shila.
Mratibu huyo aliwahimiza wafugaji wa Mkoa wa Tanga na mikoa mingine, ambayo pia ni sehemu ya walengwa wa kujenga mitambo 10,000 ndani ya miaka miwili, kuhakikisha wanaitumia fursa hii ya unafuu wa kulipia gharama za mitambo na hasa punguzo hili la bei, inayolipiwa na Wakala wa Umeme Vijijini (REA).
Akizindua mradi huo, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mwantumu Mahiza aliyewakilishwa na Ofisa Uvuvi na Mifugo, Archie Mntambo alielezea kufurahishwa kwake na uamuzi wa serikali kupitia REA kutoa Sh Sh bilioni 3.06 kutumika kutoa punguzo miongoni mwa watumiaji wa mitambo ya biogesi nchi nzima.
“Kwa kutoa fedha hizi ili kuwapa nafuu watumiaji wa nishati itokanayo na mitambo ya bayogesi, huu ni uthibitisho tosha serikali yetu inawajali wafugaji na inafanya kila juhudi kuona kuwa wanaboresha viwango vya maisha na hivyo kufanikiwa kujitoa katika lindi la umasikini wa kupitiliza. “Lakini jambo lingine lililonivutia zaidi ni kwa marafiki zetu wa Serikali ya Uholanzi kutoa Sh bilioni sita ili kutekeleza mradi huu, hii ni ishara kuwa mataifa yetu haya ni rafiki na yanajikita katika kuona kuwa maisha ya Watanzania yanaboreshwa zaidi na zaidi,” alisisitiza mkuu huyo wa mkoa.
Mkulima na mfugaji, Elibariki Kishia (74) aliyejenga mtambo wake kwa Sh 980,000 wakati wa utekelezaji wa awamu ya kwanza ya TDBP kati ya mwaka 2009 hadi 2015, alisema mtambo huo umebadili maisha yake, kwani mazao anayozalisha shambani yameongezeka kutokana na kutumia mbolea bora itokanayo na kinyesi cha ng’ombe, kilichochakatwa katika mtambo wa biogesi.
CHANZO ; HABARI LEO.

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa