Home » » MRADI WA SECAP LUSHOTO HATARINI KUTOWEKA

MRADI WA SECAP LUSHOTO HATARINI KUTOWEKA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
MRADI wa Hifadhi ya Mmomonyoko wa Udongo na Kilimo ijulikanayo kama ‘Soil Erosion Control and Agroforest Project (SECAP), unaojumuisha vijiji saba vya Mlalo na Lushoto uko kwenye hatari ya kutoweka endapo hatua za haraka kuunusuru hazitachukuliwa.
Mradi huo ulianzishwa mwaka 1980 na ulikuwa na malengo ya kuhifadhi vyanzo vya maji, kuendesha kilimo cha kisasa na kupanda miti, ambako ulilenga eneo la maili 610 hadi 2300 kwa kuwashirikisha wananchi zaidi.
Imedaiwa kuwa, wafanyabiashara wanaovuna miti katika hifadhi za miti za mradi huo hutoa kiasi cha sh 500,000 hadi sh milioni 1 kwa baadhi ya viongozi, kuhakikisha wanawalinda na mbao zao kwa madai walishaweka mambo sawa kwa baadhi ya wajumbe wa kamati ya uvunaji Wilaya ya Lushoto.
Mkurugenzi wa Halimashauri ya Wilaya ya Lushoto, Jumanne Shauri, Mwenyekiti wa Halimashauri hiyo, Lucas Shendolwa na Mbunge Henry Shekifu, wameahidi kuchukua hatua za haraka kuzuia uharibifu huo wa mazingira kuendelea walipozingumza na Mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu kwa nyakati tofauti.
Tanzania daima ilipotembelea vijiji hivyo, ambavyo ni Hemtoye, Msale, Kifulio, Makole, Kwekanga, Kihifu na Kigulunde, ilishuhudia wafanyabiashara zaidi 15 wakikata miti katika msitu huo.
Uchunguzi umeonyesha kuwa, wafanyabiashara hao waliomba vibali vya kukata miti aina ya ‘Kaltas’ kwa maelezo kuwa imekuwa ikitumia maji mengi ardhini, jambo ambalo limetoa upenyo kukata miti ya mivule na mingineyo na hakuna mapato yanayonufaisha vijiji husika.
Mkuu wa wilaya hiyo, Majid Mwanga, alisema kuwa yeye kama mwenyekiti wa kamati ya uvunaji wilaya, amekuwa akitoa vibali vya uvunaji miti baada ya kupata taarifa kutoka ngazi za vijiji na Idara ya maliasili na kwamba, mtu anapokiuka ni vema watendaji na wananchi wampe taarifa.
“Mimi niko hapa ofisini sijui nini kinatokea msituni huko…nawaomba wananchi wenye mapenzi mema kama nyinyi waandishi, mtupatie taarifa na kama wabovu ni maliasili, viongozi wa vijiji, kata au idara ya misitu… tutachukua hatua kama serikali,” alisema.
 Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Tanga Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa