Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
UKOSEFU wa gari la wagonjwa katika kituo cha afya Pongwe kilichopo
kwenye Halmashauri ya Jiji la Tanga unasababisha mazingira magumu ya
kuwasafirisha wagonjwa wanaohitaji huduma zaidi za kimatibabu kutoka
maeneo ya mbali na kituo hicho.
Akizungumza katika hafla fupi ya wafanyakazi kujipongeza kwa
mafanikio waliyopata kwa utoaji wa huduma bora zikiwemo za wajawazito
na watoto jana, Mganga Mfawidhi wa kituo hicho, Dk. Faisal Ali, alisema
wamepokea wagonjwa kutoka vijiji mbalimbali na baadhi yao kuwa na kesi
za kupata tiba hospitali nyingine, hivyo huwa vigumu kuwasafirisha.
“Hiki kituo unaweza kukiona ni kidogo ila kiutendaji ni kikubwa,
hakuna mtu ambaye hajui kama tunahudumia mamia ya watu kwa siku, tatizo
ni pale mgonjwa au mjamzito tunapotaka kumpeleka Hospitali ya Bombo
ndiyo balaa, hatuna gari,” alisema Dk. Ali.
Aliiomba serikali kupeleka gari la wagonjwa katika kituo hicho ili
kukabiliana na changamoto za wajawazito wakati wa kujifungua na utoaji
wa elimu ya umuhimu wa kuhudhuria kiliniki.
Kwa mujibu wa Dk. Ali, baadhi ya wanawake hasa wa vijijini hawajui
umuhimu wa kuhudhuria kliniki ili kujua mwenendo wa ujauzito.
Akizungumza katika hafla hiyo, Katibu Msaidizi Afya wa Halmashauri ya
Jiji la Tanga, Yombo Shelufumo, aliwataka wafanyakazi hao kutobweteka
na mafaniko waliyoyapata na kuwaasa kufanya kazi kwa bidii ili
kuyafikia mafanikio zaidi.
Alisema mbali ya changamoto nyingi wanazokabiliana nazo, zikiwemo za
kupandishwa vyeo na umbali wa wafanyakazi wanapoishi, serikali
inatambua na hivyo kuwataka kufanya kazi kwa bidii.
Shelufumo alisema siri ya mafaniko ni kufanya kazi kwa bidii, na
hivyo kuwataka kufanya uvumilivu huku serikali ikitambua changamoto
hizo na kuzifanyia kazi zikiwemo za kuwapandisha vyeo.
Chanzo;anzania Daima
0 comments:
Post a Comment